Katika kipindi ambacho ongezeko la joto duniani na viwanda vinatishia maeneo ya misitu, Türkiye imeorodheshwa miongoni mwa nchi zilizoongeza sana maeneo yake ya misitu kati ya 2015 na 2025. Kwa mujibu wa tathmini ya hivi karibuni ya Rasilimali za Misitu ya Kimataifa iliyotolewa na Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO), dunia ina jumla ya ekari bilioni 4.14 za misitu, sawa na asilimia 32 ya eneo lote la ardhi duniani, huku ekari 0.50 zikiwa za kila mtu. Sehemu kubwa ya misitu hii, karibu asilimia 45, iko kwenye maeneo ya tropiki.
Ripoti hiyo inaongeza kuwa upotevu wa misitu duniani umepungua katika miaka ya hivi karibuni. Katika kipindi cha 1990-2000 dunia ilipoteza wastani wa ekari milioni 10.7 za misitu kila mwaka, lakini hivi sasa wastani huu umeshuka hadi ekari milioni 4.12 kwa mwaka katika kipindi cha mwisho cha muongo mmoja. Pamoja na mafanikio haya, nchi za Amerika Kusini na Afrika bado zinakumbana na viwango vikubwa vya upotevu wa misitu.
Kwa mujibu wa ripoti, China inaongoza duniani kwa kuongeza eneo la misitu kwa ekari milioni 1.686 kwa mwaka, ikifuatiwa na Urusi na India, huku Türkiye ikiwa ya kwanza Ulaya na ya nne duniani kwa kuongeza wastani wa ekari 118,000 kila mwaka. Kwa upande mwingine, Brazil inaongoza kwa upotevu wa misitu, ikipoteza karibu ekari milioni 2.942 kwa mwaka. Ripoti pia inaonyesha kuwa moto, wadudu, magonjwa na matukio ya hali ya hewa kali ni visababishi vikuu vya uharibifu wa misitu, huku asilimia 20 ya misitu duniani ikiwa inalindwa kisheria.

Toa Jibu